Jumamosi asubuhi tarehe 15.11.2025
Luka 12:35-40
35 Viuno vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe zinawaka;
36 nanyi iweni kama watu wanaomngojea bwana wao, atakaporudi kutoka arusini, ili atakapokuja na kubisha, wamfungulie mara.
37 Heri watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha. Amin, nawaambieni, atajifunga na kuwakaribisha chakulani, atakuja na kuwahudumia.
38 Na akija zamu ya pili, au akija zamu ya tatu, na kuwakuta hivi, heri watumwa hao.
39 Lakini fahamuni neno hili, Kwamba mwenye nyumba angalijua saa atakayokuja mwivi, angalikesha, wala asingaliacha nyumba yake kuvunjwa.
40 Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu.
Tuvumilie hata mwisho katika Bwana;
Yesu anaongelea utumwa "mwaminifu" kwa wanafunzi wake. Anawaambia viuno vyao viwe vimefungwa na taa zao ziwe zinawaka. Wawe kama wamngojeao bwana wao kutoka harusini ili akirudi wamfungulie. Yesu anaendelea kusema ni Heri watumwa ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha kumngoja usiku kucha.
Yesu alikuwa anawaambia wanafunzi wake kumshika yeye katika maisha yao na katika utume wao. Alilenga kuwaambia wakae katika yeye hata kama atakuwa ameondoka. Ndiyo maana anamalizia kwa kusema jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo mwana wa Adamu. Nasi tujiweke tayari, kwa kuwa saa tusiyodhani Yesu yuaja. Amina
Jumamosi njema
Heri Buberwa Nteboya
0784 968650
