Alhamisi asubuhi tarehe 05.06.2025
Mwanzo 18:27-33
27 Ibrahimu akajibu, akasema, Basi, nimeshika kusema na Bwana, nami ni mavumbi na majivu tu.
28 Huenda wakapunguka watano katika wale hamsini wenye haki, je! Utaharibu mji wote kwa kupungua watano? Akasema, Sitauharibu, nikiona humo arobaini na watano.
29 Akazidi tena kusema naye, akinena, Huenda wakaonekana humo arobaini? Akasema, Sitafanya kwa ajili ya hao arobaini.
30 Akasema, Bwana asiwe na hasira, nami nitasema, Huenda wakaonekana huko thelathini? Akasema, Sitafanya, nikiona humo thelathini.
31 Akasema, Tazama, nimeshika kusema na Bwana, huenda wakaonekana huko ishirini? Akasema, Sitaharibu kwa ajili ya hao ishirini.
32 Akasema, Bwana asiwe na hasira, nami nitasema mara hii tu, Huenda wakaonekana huko kumi? Akasema, Sitaharibu kwa ajili ya hao kumi.
33 Basi Bwana alipokwisha kuzungumza na Ibrahimu, akaenda zake; Ibrahimu naye akarudi mahali pake.
Mungu husikia maombi yetu;
Sura ya 18 inaanza kwa ahadi ya Ibrahimu kupokea mtoto. Baada ya ahadi hii, wageni walioleta ahadi walielekea Sodoma, Ibrahimu akifuatana nao. Lakini Ibrahimu alikaa mbele ya Bwana, akapewa ujumbe wa Sodoma na Gomora kuangamizwa. Ibrahimu ndipo anamuomba Bwana wasiangamizwe angalau kukiwa na watu hamsini wanaomcha Bwana.
Ibrahimu aliendelea kuomba Sodoma na Gomora kusiangamizwe kama wako arobaini na tano wanaomcha Bwana, wakakosekana. Akaomba wawe arobaini, mara thelathini, mara ishirini hadi kumi kama tulivyosoma, wakakosekana.
Bwana alikuwa anaonesha huruma yake kutoiangamiza Sodoma na Gomora iwapo kungekuwa na watu hata wachache wanaomcha. Huruma ya Bwana iko hata sasa, ndiyo maana husikia maombi yetu. Omba, Mungu anakusikia. Amina
Siku njema
Heri Buberwa