Alhamisi asubuhi tarehe 03.07.2025
Yeremia 7:26-32
26 Lakini hawakunisikiliza, wala kutega sikio lao; bali walifanya shingo yao kuwa ngumu; walitenda mabaya kuliko baba zao.
27 Nawe utawaambia maneno hayo yote; lakini hawatakusikiliza, nawe utawaita; lakini hawatakuitikia.
28 Nawe utawaambia, Taifa hili ndilo lisilosikiliza sauti ya Bwana, Mungu wao, wala kupokea mafundisho; uaminifu umepotea, umekatiliwa mbali na vinywa vyao.
29 Zikate nywele zako, Ee Yerusalemu, uzitupe, Ukafanye maombolezo juu ya vilele vya milima; Kwa maana Bwana amekikataa na kukitupa Kizazi cha ghadhabu yake.
30 Maana wana wa Yuda wametenda yaliyo maovu machoni pangu, asema Bwana; wameweka machukizo yao ndani ya nyumba hiyo, iitwayo kwa jina langu, hata kuitia unajisi.
31 Nao wamepajenga mahali palipoinuka pa Tofethi, palipo katika bonde la mwana wa Hinomu, ili kuwateketeza wana wao na binti zao motoni; jambo ambalo mimi sikuliagiza, wala halikuingia moyoni mwangu.
32 Basi angalieni, siku zinakuja, asema Bwana, ambazo katika siku hizo halitaitwa tena Tofethi, wala Bonde la mwana wa Hinomu bali litaitwa, Bonde la Machinjo; maana watazika watu katika Tofethi, hata hapatakuwapo mahali pa kuzika tena.
Wito wa kuingia Ufalme wa Mungu;
Somo la asubuhi hii ni sehemu ya tangazo la Nabii Yeremia kuhusu hukumu ya Mungu kwa watu ambao walikosa utii kwa Mungu. Yeremia anaongea na watu ambao hawakumsikiliza Mungu, wakatenda mabaya kuliko baba zao. Lakini Yeremia kama alivyotumwa anawaambia kwamba kwa kutotii walikuwa wamepotea, kwa kuwa Bwana alimtuma kusema kuwa walitenda yaliyo maovu machoni pake.
Yeremia anatoa angalizo la hukumu ya Mungu kwao. Onyo la Mungu kwa Israeli lilikuwa sawa, maana baadaye walikwenda uhamishoni! Kutomsikia Bwana na kumcha kuliwafanya watolewe kwenye nchi yao na kwenda kuishi kwingine! Kutomsikia Kristo ni hatari maana ni njia ya kupotea na kuukosa uzima wa milele. Amina
Siku njema
Heri Buberwa